Home Top Ad

Responsive Ads Here

misingi ya ujamaa na Azimio la Tabora

AzimioLaArusha@50: Kuhuisha Misingi ya Ujamaa Kupitia Azimio la Tabora

Sehemu ya Hotuba ya Ndugu Zitto Juu ya Umuhimu wa Miaka 50 ya Azimio la Arusha wakati wa Uzinduzi wa Azimio la Tabora

Ndugu Wanatabora
Ndugu zangu Watanzania

Kwa takribani miaka 25 nchi yetu ilitekeleza Azimio la Arusha. Nchi yetu ilianza kujenga uchumi wa kijamaa na kujenga Taifa lenye usawa na lisilo la kinyonyaji, Taifa lisilo na ubaguzi wa aina yeyote. Taifa lililopiga vita udini na ukabila. Ili kumilikisha uchumi kwa wananchi, Serikali ilitaifisha mabenki, migodi, kampuni za bima na biashara nyingine mbalimbali za ndani na biashara ya nje.

Katika kipindi hiki pia Serikali ilijenga viwanda mbalimbali, hususan viwanda vya kuongeza thamani ya Mazao yetu ya kilimo kama vile viwanda vya nguo ikiwemo viwanda vya kuchambua pamba, viwanda vya nyuzi na nguo. Jumla ya viwanda 12 vya nguo vilijengwa nchini na kuzalisha maelfu ya ajira kwa wananchi.

Serikali pia ilianzisha viwanda vya ngozi, vya kubangua korosho, vya kuzalisha sukari, vya kubangua na kusaga kahawa, vya kamba za katani na magunia ya katani na kadhalika. Serikali pia ilijenga viwanda vikubwa 2 vya kutengeneza vipuri.

Kimsingi mpaka mwaka 1978, kabla tu ya vita vya Kagera, nchi yetu ilikuwa katika hatua ya ‘take-off’ kama wachumi tunavyoita. Waasisi wetu wa Taifa walitaka kuondokana na uchumi wa kuzalisha malighafi tu.

Yote haya tuliyafanya kwa pamoja kama Taifa ama kwa kutumia fedha zetu wenyewe za kodi au kwa kutumia mikopo na misaada kutoka nje. Hata hivyo, baada ya vita vya Kagera uchumi wetu ulianza kuporomoka na nchi yetu kulazimishwa kufuata masharti ya Shirika la Fedha la Dunia (IMF) na Benki ya Dunia".

Wakati shabaha ya Azimio la Arusha ilikuwa ni kuodokana na onyo hili la mchumi Gottob von Justi, kuanzia mwaka 1992 Tanzania ilianza kuvunjavunja misingi ya Azimio la Arusha na kurudi miaka 25 nyuma. Kimsingi uvunjaji ulianza kidogo kidogo kuanzia mwaka 1986 na ndio maana mwaka 1987 hapakuwa na tathmini iliyowazi ya Azimio kama ilivyokuwa mwaka 1977.

Ni wajibu wetu kuhakikisha kuwa mwaka 2017 tunaadhimisha miaka 50 ya Azimio la Arusha kwa kufanya tathmini ya miaka 25 ya utekelezaji wa Azimio na Miaka 25 ya kutupwa kwa Azimio. Chama cha ACT Wazalendo kinaanza mchakato huo sasa kwa kutangaza Azimio la Tabora linalohuisha Azimio la Arusha"

Kabwe Z. Ruyagwa Zitto
Kiongozi wa Chama - ACT Wazalendo
Juni, 2015
Tabora

Tanbihi: Nachukua nafasi hii kuwajulisha kuwa Machi 25, 2017 chama chetu kitafanya Mkutano Maalum wa Kidemokrasia wa maadhimisho ya miaka 50 ya Azimio la Arusha kama tulivyoahidi. Mkutano husika utafanyika jijini Arusha. Tunatarajia kuyatumia maadhimisho haya kujadili masuala ya kisera na kueleza mustakabali wa uchumi wa nchi yetu na Afrika kwa ujumla, tukikusanya wageni wa ndani na nje ya Tanzania. Punde Ukumbi na taratibu za kuhudhuria na kushiriki zitatangazwa.


misingi ya ujamaa na Azimio la Tabora misingi ya ujamaa na Azimio la Tabora Reviewed by pongwa trading on 00:49:00 Rating: 5

No comments

Recent